Hata wangemuua Kibanda atakuja mwingine


Edson Kamukara

“KAKA poleni sana kwa tukio la Absalom Kibanda. Daima msiwaogope wawezao kuua mwili ila yule awezaye kuuwa mwili na roho pia. Sina ushahidi ndugu yangu ila naamini kabisa hivyo ni vitisho vinavyotolewa na magenge ya watu wenye nia mbaya na nchi yetu tukufu.
“Naomba niwatie moyo waandishi wa habari endeleeni kupambana kwa kutumia kalamu yenu, waacheni wao waendelee kutumia bisibisi, mapanga, marungu na risasi za moto ila mwisho wa siku mkweli atabaki salama.
“Watamuua Kibanda atabaki Edson, watamuua Edson atakuja mwingine, daima hawataisha wote. Si siri tukio alilofanyiwa Kibanda limenisikitisha sana, limenisononesha sana, limenihuzunisha sana na mwisho wa siku moyo wangu umejaa ghadhabu, hasira na chuki kubwa sana.”
Haya ni maneno ya faraja kutoka kwa rafiki yangu wa mkoani Tanga, siku moja baada ya mwenzetu Mhariri Mtendaji wa Kampuni ya New Habari (2006) Ltd ambao ni wachapishaji wa magazeti ya Rai, Mtanzania, Dimba na Bingwa, Absalom Kibanda kuvamiwa na watu wasiojulikana nyumbani kwake eneo la Mbezi Beach nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam kisha kupigwa na kujeruhiwa vibaya.
Kibanda ambaye pia ni Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) alipigwa na kitu kizito chenye ncha kali kichwani, kutobolewa jicho la kushoto, kunyofolewa ukucha na kukatwa kidole cha mkono na kung’olewa meno mawili.
Hakika ni tukio la kuhuzunisha, kutisha na zaidi ni unyama unaotendwa na binadamu wenzetu ili kuendelea kukidhi ajenda zao binafsi. Niseme kuwa Mungu ni wetu sote na hivyo iko siku makatili hawa wataumbuliwa.
Hili ni tukio la kutia hofu na kuacha mashaka mengi kwani linakuja ikiwa ni miezi takriban tisa tangu kutekwa, kuteswa, kuumizwa vibaya, kung’olewa meno na kucha na kutelekezwa msituni Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari nchini, Dk. Stephen Ulimboka, usiku wa Juni 26, mwaka jana.
Tangu kutekwa na kuteswa kwa Dk. Ulimboka katika mazingira yanayofanana na tukio la Kibanda, Jeshi la Polisi nchini limekuwa likitupiana mpira katika kueleza hatua zilizofikiwa kuwasaka waliohusika.
Licha ya mtuhumiwa pekee raia wa Kenya, Joshua Mulundi kufikishwa mahakamani akidaiwa kuhusika na tukio hilo, bado polisi imeshindwa kumhoji Dk. Ulimboka wala watuhumiwa aliowataja kwa majina kuwa walihusika kumteka na kumtesa.
Kibanda kwa sasa amehamishiwa katika Hospitali ya Milpark nchini Afrika Kusini kujaribu kuokoa maisha yake, madaktari wamemfanyia vipimo mbalimbali vikiwamo CT Scan na X-ray hasa kichwani na sehemu nyingine za mwili ambazo zilipata majeraha.
Tumeelezwa kuwa imebainika kwamba mfupa laini (fizi) uliopo kati ya pua na mdomo ni kama umekatika. Hii inatokana na nguvu na nyenzo walizotumia watesaji kumng’oa meno. Kutokana na hali hiyo ana maumivu makali sana kwenye kinywa chake.
Pia imebainika kwamba meno kama sita hivi katika kinywa chake yamelegea. Kwamba haya ni tofauti na yale mawili yaliyong’olewa katika tukio la awali.
Narudia tena kusema kuwa ni unyama na mkakati wa binadamu wenzetu wasiothamini uzalendo na uhai wa wengine. Hawa wako tayari kufanya lolote ili mradi mambo yao yanyooke. Wataendelea kututesa kama walivyofanya kwa Kibanda lakini watambue huo si mwisho wa mapambano.
Tunahuzunika, tunalaani tukio la Kibanda lakini shaka haituishi kwani hatuoni juhudi za kukomesha vitendo vya mateso na mauaji kwa waandishi wa habari.
Mara kwa mara tunasikia salamu za pole na rambirambi zikipitishwa kwetu kwenda kwa watu mbalimbali waliopata matatizo lakini kwa mwandishi mwenzetu marehemu Daudi Mwangosi hizo salamu hazikuwepo na sasa Kibanda naye hali ni hiyo hiyo. Magwiji wa kufariji kila tukio wamekaa kimya kama hawapo.
Simaanishi kwamba tunahitaji pole zao wakati tunakufa na kuteswa wakifurahia, isipokuwa nataka umma wa Watanzania tunaoutumikia utambue kuwa wanahabari wa Tanzania tunafanya kazi hatarini, kifo na mateso yetu ni wakati wowote. Hatujui nani atafuata baada ya Kibanda.
Kama Kibanda alifanyiwa unyama huo langoni kwake ni dhahiri kuwa watatuwinda hata barabarani, wakiamua watatufuata ofisini kama walivyowafanyia Saed Kubenea na Ndimara Tegambwage wa gazeti la MwanaHalisi.
Kibanda ameteswa wakati akikabiliwa na kesi ya uchochezi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu. Anashitakiwa na Jamhuri akidaiwa kuchapisha makala katika gazeti hili la Tanzania Daima wakati akiwa Mhariri Mtendaji wake.
“Baada ya kuona hali hiyo nilitaka kujiokoa kwa kukimbia lakini nilianguka, hivyo wakaanza kunishambulia kwa kunipiga nondo kichwani na sehemu mbalimbali za mwili, wakanikata kidole kwa kuing’oa kucha na kunitoboa jicho la kushoto,” haya ni maneo ya Kibanda akiwa hospitalini Muhimbili.
Katika masikitiko haya, nafurahi kuwa umma wa wananchi uko nyuma yetu, unatupa matumaini ili tusife moyo kwa vitisho na vitendo viovu tunavyofanyiwa. Swali na kujiuliza ni nani wanafanya unyama huu, wanaatumwa na nani, kwa sababu gani na wanalipwa nini?
Haya ni baadhi ya wasomaji wa gazeti letu, walioguswa na tukio la kuteswa kwa Kibanda. Kwa kuwa sikuwajulisha kama nitayachapisha, nitaomba nisiwataje majina yao wala namba zao za simu.
“Ukweli kuhusu kuteswa na kuumizwa kwa jamaa yetu Kibanda kamwe hauwezi kupatikana kupitia kamati za vyombo vya kiserikali ikiwemo polisi ambayo mara zote imekuwa mtuhumiwa wa kwanza. Mwangalieni sana au mchunguzeni huyo wanayemwita …(anamtaja kigogo mmoja).
“Hiyo ni desturi yake hata katika chaguzi za kata huku zimewaacha watu wengi vilema, kazi yake ni kufadhili ‘janjaweed’ katika miaka yote anayoshinda, ameumiza sana watu.” 0757******
“Kama kweli polisi wanasema wanahitaji ushirikiano wenu, basi ni muda muafaka wa kumwambia IGP Said Mwema kuwa kwa vile mbinu za mateso ni zile zile kama zilizotumiwa kwa Dk. Stephen Ulimboka basi watu waliotajwa na Ulimboka wawe wa kwanza kukamatwa na kuwekwa ndani wakiwa wanangojea ushahidi wa Kibanda kutoka hospitali, vinginevyo, kinachofanyika ni usanii.” 0756******

“Kwanza natoa pole kwa timu nzima ya wanahabari kwa matukio yanayowakabili ambayo yanatishia usalama wenu katika utekelezaji wa majukumu yenu, pili niwaombe muwe na ushirikiano katika kipindi hiki kigumu ili huyu adui anayewaandama apatikane.
“Serikali inawajua ilisajili laini za simu ili kubaini matumizi mabaya ya simu, hawa wanaowatishia wamiliki wa namba hizo wanatoka Ulaya? Nimeguswa sana na mateso aliyoyapata Kibanda.” 0718******
“Pole sana kwa yaliyomkuta Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri, Kibanda. Mimi kama mwananchi ambaye nimekuwa nikifuatilia makala zake kwa kweli inaniuma na hasa kuona vitendo kama hivi vinazidi kushamili kwa waandishi wa habari na hatua hazichukuliwi. Tunawaombea uzima bila shaka atapona.” 0713******
“Poleni jamani, naona hii kazi sasa inakuwa na maadui wengi, kuwa makini kaka yangu.” 0713******
Hii ndiyo Tanzania waliyotuachia wazee wetu Nyerere, Mwinyi na Mkapa? Tunakwenda wapi kama tumeruhusu kutekana, kuumizana na hata kuuana? Tafakari!
Share this article :
 
Support : Creating Website | SAMBA Template | HAKI LEO Template
Copyright © 2011. HAKI LEO - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by HAKI LEO Template
Imewezeshwa na Haki Leo Company