Madiwani wa Chadema waapishwa

www.hakileo.blogspot.com

HATUA ya madiwani wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kuapishwa kisha kushiriki hafla ya kukabidhi msaada watoto wanaoishi katika mazingira magumu, imetajwa kufufua upya ushirikiano. Kuapishwa kwa madiwani wanne walioshinda katika uchaguzi mdogo kulifanyika jana, katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya Jiji la Arusha.

Madiwani hao walikula kiapo mbele ya Hakimu Mkazi, Hawa Mguruta, huku Mwanasheria wa Jiji, Alan Ndomba na Kaimu Mkurugenzi wa Jiji, Elfas Mollel wakishuhudia tukio hilo.

Walioapishwa ni Diwani wa Kata ya Kimandolu, Rayson Ngowi, Diwani wa Kata ya Erelai, Mhandisi Jeremiah Mpiga, Diwani wa Kata ya Themi, Edmund Kinabo na Diwani wa Kata ya Kaloleni, Emmanuel Kessy.

Baada ya kula kiapo madiwani hao walishiriki hafla iliyofanyika mbele ya jengo la Mkuu wa Mkoa wa Arusha na kushiriki tukio hilo la kijamii na Mwakilishi wa Ubalozi wa Falme za Kiarabu, Bader Nahdi.

Katika halfa hiyo, madiwani hao walikutana na Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Magesa Mulongo, Meya wa Jiji la Arusha, Gaudence Lyimo na madiwani wa CCM, ambapo walizungumza na kubadilishana mawazo.

Diwani Ngowi akizungumza katika hafla hiyo, alisema kuapishwa kwake kumekamilika na sasa ni muda wa kufanya kazi za wananchi.

“Siasa na muda wa kufanya kampeni umekwisha, kilichobakia ni kuwatumikia wananchi kwa kufanya kazi kwa bidii matokeo ya kazi yaonekane,” alisema Ngowi.

Kwa upande wake, Diwani Mpiga, aliomba ushirikiano kwa madiwani wote kufanya kazi, kwa kuwa wote wamechaguliwa na wananchi kwa kura.

“Sote tumechaguliwa na wananchi hakuna sababu ya kugongana tufanye kazi tuwaletee maendeleo wananchi wetu,” alisema Mpiga.

Naye, Diwani wa Kata ya Themi, Kinapo, alisema tofauti ya vyama sasa imemalizika, kilichobakia ni kuwapigania wananchi bila kuonyesha itikadi za vyama vya siasa. 

Kwa upande wake, Meya wa Jiji la Arusha, Lyimo, aliyekuwa akisalimiana nao mmoja baada ya mwingine, huku wakionyesha furaha, aliwapongeza kwa ushindi walioupata.

“Hongereni kwa ushindi mmetupiga. Lakini naomba sasa tufanye kazi tuwaletee watu wetu maendeleo,” alisema Lyimo.
Share this article :
 
Support : Creating Website | SAMBA Template | HAKI LEO Template
Copyright © 2011. HAKI LEO - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by HAKI LEO Template
Imewezeshwa na Haki Leo Company