
Victoire Ingabire, akiwa na wakili wakeAFP PHOTO/Steve Terrill
Na Flora Martin Mwano
Mahakama kuu nchini Rwanda imemuhukumu kifungo cha miaka 15 jela kiongozi wa Upinzani nchini Rwanda Bi. Victoire Ingabire Umuhoza anayekabiliwa na kosa la uhaini. Hukumu hiyo imetolewa baada ya mwanasiasa huyo kukata rufaaa kupinga kifungo cha miaka nane alichokuwa akikabiliwa nacho hapo kabla.
Mahakama imethibitisha tuhuma zinazomkabili mwanasiasa huyo ambao ni ugaidi, kukuza chuki baina ya Wanyarwanda na kuhusika na mauwaji ya halaiki dhidi ya wanyarwanda kutoka jamii ya watutsi yaliotokea mwaka 1994.
Awali Ingabire alihukumiwa kifungo cha maisha jela baada ya kupatikana na hatia ya kutenda makosa ya uhaini kutokana na kufadhili vikundi vya kigaidi pamoja na kushiriki kwenye mauaji ya kimbari ya mwaka 1994 ambayo yalisababisha vifo vya zaidi ya watu laki nane nchini humo huku wengi wao wakiwa ni Watutsi.
Baadaye alipata msamaha wa Rais na kifungo chake kupunguzwa hadi miaka nane, na baada ya rufaa ya sasa kifungo hicho kimeongezeka hadi miaka 15.
Ingabire ambaye ni mpinzani mkubwa wa Rais Paul Kagame, aliwekwa jela tangu mwezi Oktoba mwaka 2010 na ameendelea kusisitiza kutotenda makosa ambayo yameelekezwa kwake akidai kile kinachofanyika kinamsukumo wa kisiasa.
Ingabire ambaye ni Mhutu na Kiongozi wa Chama Cha FDU alirejea nchini Rwanda mwaka 2010 mnamo mwezi Januari baada ya kuishi uhamishoni nchini Uholanzi baada ya kutajwa kuhusika kwenye mauaji ya kimbari ya mwaka 1994.
