
Watu wenye silaha wameishambulia kwa silaha ngome ya vikosi vya Ufaransa huko kaskazini mashariki mwa Mali. Duru za kijeshi nchini Mali zimeeleza kuwa, kundi moja la watu wenye silaha wasiojulikana limeishambulia ngome ya majeshi ya Ufaransa na vikosi vya kulinda amani vya Umoja wa Mataifa MINUSMA mjini Kidal. Viongozi wa jeshi la Ufaransa nchini humo wamethibitisha kutokea shambulio hilo na kuongeza kuwa halikuwa na maafa. Shambulizi hilo limetokea kufuatia kuongezeka machafuko ya tangu wiki kadhaa zilizopita huko kaskazini mwa nchi hiyo ya magharibi mwa Afrika. Siku chache zilizopita pia askari wawili wa kulinda amani wa Umoja wa Mataifa raia wa Senegal wameuawa kwa mripuko wa bomu lililokuwa limetegwa ndani ya gari mjini Kidal. Mbali na askari hao wawili kuuawa, mripuko huo uliwajeruhi vibaya pia askari wa gadi ya taifa ya Mali na wale wa kikosi Umoja wa Mataifa, MINUSMA.
