Kama ilivyokuwa baada ya mauaji ya Padri
Mushi, taarifa kutoka ndani ya jeshi la polisi zimeeleza kuwa washukiwa
wa mauaji ya Imamu huyo, hawakujulikana.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa Kaskazini
Unguja, Ahmada Khamis, aliimbia NIPASHE Jumapili kuwa Imamu huyo
alichomwa kwa kifaa hicho kinachosadikiwa kuwa kisu, majira ya saa 8.30
mchana, alipokuwa shambani kwake Kitope.
Ahmada alisema Sheikh Ali alikwenda
shambani kwa nia ya kukagua mazao yake, kwa bahati mbaya akakutana na
watu waliokuwa wakiangusha na kuiba nazi zilizopo shambani humo.
Alisema, uchunguzi wa awali wa polisi
umebaini kutokea kurupushani kati yake (Imamu) na watu wanasaidikiwa
kuwa wezi wa nazi na ndipo Sheikh akashambuliwa kwa kitu chenye ncha
kali shingoni na kufa papo hapo.
“Tumeanza kufanya uchunguzi ili kuwakamata
watuhumiwa waliohusika na mauaji hayo ili wafikishwe katika vyombo vya
sheria,” alisema Ahmada.
Ahmada alisema mazingira ya eneo
lilipotokea tukio hilo, yameonyesha kuwa, kabla ya kufanyika,
waliangusha nazi, kufua na kuacha makumbi ndani ya shamba.
Hata hivyo, alisema ni vigumu
kulilinganisha tukio hilo na vitendo vya hujuma na kuandamwa kwa
viongozi wa dini kulikojitokeza hivi karibu visiwani Zanzibar.
Daktari aliyefanya uchunguzi wa mwili wa
marehemu Sheikh Ali, Dk. Msafiri Marijani wa hospitali ya rufaa ya Mnazi
Mmoja, alisema alikufa kutokana na kupoteza damu nyingi baada ya
kuchomwa kisu upande wa kulia wa shingo yake.
Dk. Marijani alisema, mzunguko wa damu
uliathirika kutokana na kina cha ncha kali kuuathiri mshipa mkubwa wa
damu, hivyo kusababisha (damu) kuvuja kwa wingi.
“Uwezekano wa kupona kwa Sheikh Ali
ulikuwa ni mdogo kutokana na ukubwa wa jereha alilolipata shingoni
kwake, baada ya kupigwa na kitu kinachoaminika ni kisu kikali, ”alisema
Dk. Marijani.
Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja, Pembe
Khamis Juma, alisema baada ya uchunguzi wa kitaalam kufanyika,
wanafamilia walikabidhiwa mwili wa marehemu kwa ajili ya maandalizi ya
mazishi.
Pembe alisema marehemu alikuwa ni mkaazi
wa Mwakaje, aliyemiliki shamba huko Kitope na tayari vyombo vya dola
vimeanza kufanya uchunguzi ili kufahamu ukweli wa tukio hilo.
Tukio la kuuawa Sheikh Ali, limekuja huku
Zanzibar ikiandamwa na matukio kadhaa ya kutisha, ikiwa ni pamoja na
mfululizo wa viongozi wa dini kuhujumiwa na kuuawa.
Viongozi waliohujumiwa ni Katibu wa Mufti
Sheikh Fadhil Soraga aliyemwagiwa tindikali,Padri Ambrose Mkenda
aliyejeruhiwa kwa kupigwa risasi mbili shingoni na Padri Evarist Mushi
aliyepigwa risasi tatu kichwani na kuuawa Februari 17 mwaka huu.
