Hongera Kenyatta na Wakenya

http://media2.picsearch.com/is?vvTJctG36V4x5Q4vl10rxn9uOUqrnNJL3JGbDofuhDM


TUME huru ya uchaguzi nchini Kenya (IEBC), jana ilimtangaza Uhuru Kenyatta kupitia Muungano wa Jubilee kuwa mshindi wa uchaguzi mkuu uliofanyka Jumatatu wiki hii. Kenyatta ambaye anakuwa rais wa nne wa taifa hilo, alijipatia kura 6,173,433 (50.03%) na kumwangusha hasimu wake wa karibu Waziri Mkuu anayemaliza muda wake, Raila Odinga aliyejipatia kura 5,340,546 (43.28%) kati ya kura 12,338,667 zilizopigwa.
Tunampongeza Kenyatta kwa kuchaguliwa kuiongoza Kenya katika uchaguzi uliofanyika kwa hali ya amani, utulivu na uwazi wa hali ya juu, hatua inayoonesha kuwa Wakenya wameamua kuweka maslahi ya taifa lao mbele kwanza.
Tunasema hivyo kutokana na ukweli kwamba kila mgombea wa kiti hicho cha urais alikuwa mstari wa mbele kuwasisitiza wafuasi wake kutunza amani, hata pale zilipojitokeza kasoro ndogo ndogo, lengo ni kutorudia vurugu za baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2007 ambapo watu zaidi ya 1,300 waliuawa na wengine zaidi ya 600,000 kuachwa bila makazi.
Wakenya wameamua, chaguo lao ni Kenyatta na hata tume huru ya uchaguzi imejitahidi kwa kila jinsi kuweka imani kwamba kura zao hazichakachuliki.
Tumeshuhudia jinsi IEBC ilivyojaribu kuhakikisha kila kitu kinakwenda vizuri na kuondosha malalamiko ya hapa na pale, hasa pale teknolojia mpya ya kuhesabu kura kwa mashine ilivyogoma na hivyo kulazimika kuzihesabu upya kwa mikono.
Huu ni mfano wa kuigwa na nchi nyingine za bara hili la Afrika ikiwemo Tanzania, ambazo nyingi zimekuwa na chaguzi zenye mizengwe ya wizi wa kura, matumizi makubwa ya vyombo vya dola, ubabe na siasa chafu za kupakana matope.
Lakini kwa wenzetu Wakenya sera za vyama ndizo zimenadiwa na wagombea kupigiwa kura kutokana na umahiri wao. Tumeona wagombea urais wote nane waliojitokeza kila mmoja akinadi sera zake na kueleza nini atafanya akichaguliwa.
Jambo jema na la kutia moyo ni pale matokeo yalipokuwa yakiendelea kupatikana, baadhi ya wagombea walijitokeza wazi na kukiri kushindwa na hivyo kuwapongeza wenzao waliokuwa wakielekea kushinda.
Hata baada ya matokeo ya jumla kutangazwa jana, Raila alimtumia salamu za pongeza Rais mteule Kenyatta licha ya kwamba muungano wao wa Cord walikuwa katika hatua za kutafakari kupinga ushindi huo mahakamani.
Aliwasihi wafuasi wake kuwa makini, watulivu na wenye subira wakati huu wakitafakari ni hatua gani za kuchukua. Huu ni mfano wa kuigwa. Hongera Kenyatta na Wakenya kwa ujumla.
Share this article :
 
Support : Creating Website | SAMBA Template | HAKI LEO Template
Copyright © 2011. HAKI LEO - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by HAKI LEO Template
Imewezeshwa na Haki Leo Company