Sura hizi zimewakosea nini Watanzania?


Christopher Nyenyembe

IMENICHUKUA muda mrefu kujipanga ili niweze kujua kuwa nataka kuandika nini kuhusu watu hawa; Dk. Harrison Mwakyembe, marehemu Daudi Mwangosi, Danny Mwakiteleko, Absalom Kibanda na Dk. Stephen Ulimboka.
Nakumbuka ni ndani ya miezi saba nilipokuwa miongoni mwa Watanzania wachache tulioshiriki kumzika mtangazaji wa Televisheni ya Channel Ten, Daudi Mwangosi huko nyumbani kwao Tukuyu.
Nakumbuka niliposhiriki mazishi ya aliyekuwa Mhariri Mtendaji wa magazeti ya New Habari Corporation, Danny Mwakiteleko, aliyekufa kwa ajali ya gari akitokea kazini majira ya usiku kuelekea nyumbani kwake jijini Dar es Salaam. Nilishiriki mazishi yake huko Mwakaleli, Tukuyu.
Nakumbuka baada ya mazishi hayo nilipoitwa na kukutana na wazee wa Kyela ili waweze kutoa dukuduku lao na shaka kubwa ya ugonjwa uliomkumba, Mbunge wa jimbo hilo, Dk. Harrison Mwakyembe na kumsababishia madhara makubwa mwilini na hasa ngozi.
Nakumbuka jinsi wazee hao hao walivyotaka baadaye kufahamu nani aliyeweza kumdhuru kiongozi wa umoja wa madaktari, Dk. Stephen Ulimboka na kumuumiza vibaya na hatima ya uhai wake iliweza kuokolewa na madaktari bingwa nchini Afrika Kusini.
Sasa siwezi kusema tena nakumbuka isipokuwa imetokea tena, aliyekuwa Mhariri Mtendaji wa magazeti ya Tanzania Daima na baadaye kuhamia Kampuni ya New Habari na kuwa katika nafasi hiyo ya juu kwenye vyombo vya habari, Absalom Kibanda naye amefanyiwa unyama mkubwa kama Dk. Ulimboka.
Si kwamba nataka kuwataja Watanzania hao wachache kwa maana ndio walioweza kuathiriwa zaidi kwenye moja ya majukumu yao ya kutekeleza wajibu wao isipokuwa nina hoja ya msingi ya kutaka kufahamu, watu hawa wamewakosea nini Watanzania?
Ukiacha tukio lililomkuta Dk. Ulimboka kama daktari kitaaluma, narudi nyuma ili kuweza kuona na kushitushwa na matukio ya wana habari kuvamiwa, kupigwa, kujeruhiwa na wengine kuuawa katika mazingira yenye utata, hayo yametokea na hali inazidi kutia shaka zaidi.
Naanzia kwa wanahabari kwa wale wasiofahamu Dk. Harrison Mwakyembe licha ya kuwa kitaaluma ni mwanasheria pia ni mwandishi wa habari kitaaluma, kwa hali yoyote ile madhara aliyoyapata hayakuweza kufungwa na kazi yake anayoifanya sasa kama waziri pia wanahabari wanaomfahamu waliguswa na mkasa uliompata.
Katika mazingira hayo naweza kuyasukuma mawazo yangu na mawazo ya watu wengine jinsi tasnia ya habari inavyozidi kuzungukwa na maadui, tena maadui wakubwa na wenye dhamira mbaya hasa wakiwalenga watu ambao si rahisi kupona kutokana na ujasiri wao mkubwa walionao wa kupigania na kutetea masilahi ya nchi hii.
Leo hii, ‘Tuendako’ Absalom Kibanda kama ambavyo amekuwa akiwaelimisha wananchi kupitia safu yake ya Tuendako amelazwa nchini Afrika Kusini akiendelea kupatiwa matibabu baada ya kuumizwa vibaya na watu wanaojulikana, wapo na kwa kuwa wapo si kazi ya wanahabari kuwakamata hiyo ni kazi ya vyombo vya usalama.
Kuna mambo mawili ambayo kama serikali haitaweza kushtuka haraka na kutokulala usingizi, misingi ya kihabari itakuwa shakani na viongozi wa madhehebu ya dini nao hawawezi kufanya kazi zao kwa uhuru na haki ya kuabudu, waandishi wanauawa, viongozi wa dini nao wanauawa, sasa nini kifanyike?
Ni dhahiri kwamba matukio ya hivi karibuni yanayoendelea kuvaa sura ya ukatili na uvunjifu wa haki za binadamu kupita kiasi yanazidi kukua na kutishia usalama wa mamlaka za kidini na taaluma ya uandishi wa habari nikiamini katika kusema kweli makundi hayo mawili yapo hatarini.
Lazima tujiulize hawa wanaowatuma watu wawaue mapadri, wachungaji na masheikh wametoka wapi na wanafanya hivyo kwa nia ipi nzuri, kama hata wao ipo siku hawatakufa na ni kina nani hao wanaokesha kwenye nyumba za siri wanamua kuwatuma watu wawavamie waandishi wa habari, wanafanya hivyo kwa kuwa kazi wanayoifanya nao hawawezi kufa?
Ningeweza kupanga vizuri orodha ya wanahabari mmoja baada ya mwingine waliokumbwa na madhara, kufa wakiwa wanatekeleza majukumu yao, wanafanya kazi ya kuwafikishia habari wananchi, kosa lao ni nini kwa nini jamii inawahukumu wanahabari ambao ndio jicho lao?
Kuumizwa, kupigwa na kuuawa kwa wanahabari haiwezi kuwa fimbo ya mwisho katika ukombozi wa nchi inayoficha maovu yake chini ya uvungu wa kitanda, watakufa wachache lakini wengi watajitokeza na kuwa mashujaa wataweza kufichua uoza unaoitafuna nchi hii taratibu.
Ipo haja vyombo vya usalama vikafanya kazi zake usiku na mchana ili kuweza kufichua aina hii ya ukatili, mauaji na kuvuruga haki za binadamu wengine bila sababu, ndiyo maana nauliza, hivi watu hawa wamewakosea nini Watanzania?
Kuumizwa vibaya kwa Kibanda si mwisho wa uhunzi, kuuawa kwa Mwangosi si mwisho wa uhunzi, ajali ya Mwakiteleko yenye utata si mwisho wa uhunzi, madhara aliyoyapata Dk Mwakyembe si mwisho wa uhunzi na madhara wanayoendelea kuyapata wanahabari sehemu mbalimbali kwa nyakati tofauti si mwisho wa uhunzi, si usiku, si mchana ipo siku nuru ya haki itaangaza na kuwaaibisha watu wabaya wanaowadhuru wenzao.
Wanahabari hawapaswi kukata tamaa kwa kuwa penye haki Mungu husimama na penye uovu lazima wafuasi wa shetani wataangamizwa na hawawezi kufaulu kila siku, zamu yao itafika na huo utakuwa ndio ukombozi wa nchi hii, kwani damu inayomwagika haina hatia, ni ya watu wanyonge na itang’arishwa zaidi na wale wote wanaoitakia mema nchi hii. Mungu ibariki Tanzania.
Share this article :
 
Support : Creating Website | SAMBA Template | HAKI LEO Template
Copyright © 2011. HAKI LEO - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by HAKI LEO Template
Imewezeshwa na Haki Leo Company