Balozi wa Ufaransa azuiwa hafla za mauaji ya kimbari


Serikali ya Rwanda imemzuia balozi wa Ufaransa nchini humo kuhudhuria shughuli ya miaka 20 ya kukumbuka mauaji ya kimbari ya mwaka 1994.

Michel Flesch amesema kuwa, Wizara ya Mambo ya Nje ya Rwanda ilimpigia simu usiku wa jana na leo asubuhi kumfahamisha kuwa, hangeruhusiwa kushiriki kwenye shughuli hiyo iliyofanyika katika uwanja wa michezo wa Amahoro mjini Kigali. Hatua hiyo ya serikali ya Rwanda inatokana na mzozo wa hivi karibuni wa kidiplomasia kati ya nchi hiyo na Ufaransa kufuatia hatua ya Rais Paul Kagame ya kuituhumu tena Paris kuwa ilihusika na mauaji ya kimbari ya mwaka 1994. Matamshi ya Rais Kagame kwenye mahojiano na gazeti la kila wiki la Jeune Afrique linalochapishwa mjini Paris, yalipelekea Ufaransa kuamua kwamba Waziri wake wa Sheria hatashiriki shughuli ya miaka 20 ya kukumbuka mauaji ya kimbari ya Rwanda na badala yake Paris ingewakilishwa na balozi wake mjini Kigali. Wizara ya Mambo ya Nje ya Rwanda haijaelezea ni kwa nini imemzuia Balozi Michel Flesch kuhudhuria kumbukumbu za leo.
Share this article :
 
Support : Creating Website | SAMBA Template | HAKI LEO Template
Copyright © 2011. HAKI LEO - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by HAKI LEO Template
Imewezeshwa na Haki Leo Company