PINGAMIZI LA T.A.G KUZUIA ASKOFU KULOLA KUZIKWA EAGT BUGANDO LASHINDIKANA



Katika hali isiyotarajiwa hapo jana bodi ya wadhamini wa kanisa la Tanzania Assemblies of God nchini jijini Mwanza iliamua kwenda mahakamani kuwasilisha pingamizi la kutoruhusu mwili wa aliyekuwa askofu mkuu wa kanisa la E.A.G.T marehemu Dkt. Moses Kulola kuzikwa katika viwanja vya kanisa hilo lililopo maeneo ya Bugando jijini Mwanza wakidai ni mali yao jambo ambalo hata hivyo haikuwezekana na mwili huo utazikwa kama ilivyopangwa mapema hii leo.

Akizungumza na WAPO Radio Fm kupitia kipindi cha habari Yaliyotokea askofu Lameck Mkumba wa E.A.G.T amesema ameshangazwa na uamuzi huo kwakuwa waumini wa kanisa la E.A.G.T wamekuwa wakilitumia kanisa hilo la Bugando kwa muda mrefu sasa bila kuwapo matatizo yeyote hadi kuibuka kwa suala hili ambalo hawakutarajia" Mimi mwenyewe nina miaka zaidi ya 15 nikiwa muumini na niliokoka ndani ya kanisa hili la Bugando E.A.G.T" amesema askofu Mkumba

Aidha askofu huyo amesema baada ya kuona wenzao wametumia taratibu za kisheria kwakutumia bodi ya wadhamini wao mahakamani ikabidi nao pia kutafuta uwakilishi wa kisheria ambao uliwasimamia vyema kwakuwasilisha vielelezo na maelezo ya msingi ambayo mahakama iliridhika nayo nakuamua kuwapa kibali cha kuendelea na maziko ya askofu Kulola katika viwanja hivyo.

Kwa upande wake mchungaji wa kanisa la E.A.G.T City centre la jijini Dar es salaam Florian Katunzi amesema licha ya changamoto zote za kibinaadamu zilizojitokeza bado askofu Moses Kulola ataendelea kuwa shujaa wa imani nchini kutokana na kufahamika kwake vyema katika suala la injili na kulitaka kanisa kwa ujumla kukaa tayari kwakuwa Yesu anakuja na kuwataka kuachana na migongano ambayo haisaidii kanisa kusonga mbele.

Wakati huo huo askofu mkuu wa kanisa la T.A.G Barnabas Mtokambali anatarajia kuzungumza na waandishi wa habari ofisini kwake saa nne asubuhi leo kwaajili ya kutolea ufafanuzi baadhi ya mambo baada ya kuulizwa na mtangazaji wa WAPO Radio FM Beatrice Kamanga kupitia kipindi cha Yaliyotokea akitaka kujua amepokeaje hali iliyojitokeza huko Mwanza hapo jana.

Hapa ndipo atakapolala Askofu MKuu Moses Kulola
Share this article :
 
Support : Creating Website | SAMBA Template | HAKI LEO Template
Copyright © 2011. HAKI LEO - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by HAKI LEO Template
Imewezeshwa na Haki Leo Company