Pande mbili S. Kusini zimetenda uhalifu

HABARI ZETU

Ripoti ya Ivan Simonovic inatarajiwa kuwa tayari katika wiki chache zijazo
Msaidizi wa katibu mkuu wa umoja wa mataifa anayeshughulikia maswala ya haki za binadam, Ivan Simonovic, ameiambia BBC kuwa pande mbili zilizo kwenye mgogoro nchini Sudan Kusini zimehusika katika utekelezaji wa vitendo vya mauaji.
Bwana Simonovic amekuwa kwenye ziara ya maeneo mbalimbali ya Sudan Kusini ili kupata ukweli kwa ajili ya kuandaa ripoti ya Umoja wa Matifa na ameelezea kuwa ana ushahidi wa kutosha kusema pande mbili kwenye mgogoro zina hatia.

Ripoti hiyo pindi itakapokuwa tayari, ataiwasilisha kwa Baraza la usalama la umoja wa mataifa, hasa kutathimini mauaji yaliyojitokeza katika mgogoro ulioanza mwezi Disemba mwaka jana.

Maelfu ya watu wameuawa katika mwezi mmoja uliopita katika mgogoro kati ya serikali na waasi wanaoongozwa na makamu wa zamani wa Rais Riek Machar.

Bwana Simonovic aliambia BBC kwamba pande zote mbili serikali na waasi zilifanya uhalifu.

"Lakini kila upande ulihusika kwa kiwango fulani na katika maeneo tofauti. ''

Simonovic amesema kuwa maeneo yaliyoathirika zaidi, yalikuwa Mji wa Bor kusini mwa nchi hiyo na Bentiu Kaskazini mwa nchi hiyo.

Wiki jana watu 200 walikufa maji katika ajali ya boti walipokuwa wanakimbia vita

"Mji wa Bor hauna watu na Bentiu umekuwa kama mji ambao haujawahi kuishi watu. Haujaporwa bali umeteketezwa, '' alisema bwana Simonovic.

"Raia wapo kwenye kambi za wakimbizi wa ndani.Kinachochukiza ni kwamba kuna tatizo la ukabila hapa ambavyo mgogoro ulianza na nani anayewalenga raia.''

"Nadhani ni muhimu kuweza kuchunguza kwa undani chanzo cha mgogoro na pia kuripoti unyama unaotendewa raia.''

Bwana Simonovic amesema ripoti yake itakuwa tayari katika wiki chache zijazo.

Mgogoro huu ulizuka Disemba tarehe 15 wakati ambapo Rais Salva Kiir alimtuhumu aliyekuwa makamu wake wa Rais Riek Machar kwa kupanga njama ya mapinduzi dhidi ya serikali yake.

Inaarifiwa mgogoro wenyewe unaegemea zaidi upande wa ukabila. Bwana Kiir anatoka katika jamii ya Dinka yenye idadi kubwa ya watu huku Machar akitoka kabila la Nuer.
Share this article :
 
Support : Creating Website | SAMBA Template | HAKI LEO Template
Copyright © 2011. HAKI LEO - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by HAKI LEO Template
Imewezeshwa na Haki Leo Company