TAKUKURU ni mbwa koko


Salehe Mohamed

MITAANI kwetu tumewapachika jina la ‘koko’ mbwa wote wasioonesha ukali, iwe mchana au usiku, hata wanapobweka hakuna mwenye kuwaogopa.
Kimsingi mbwa wa aina hii hudharauliwa sana mitaani, hawa pia hawana matunzo mazuri kutoka kwa wamiliki wao, maana kila uchwao huzurura huku na huko kujitafutia chakula na maji.
Mbwa koko humuogopa mhalifu, akijitutumua huishia kuwasumbua watoto wadogo. Hivi ndivyo ilivyo TAKUKURU.
Taasisi hiyo huwakamata dagaa wa rushwa na kuwaacha papa na nyangumi ambao ndio wanaoitafuna nchi kwa kiasi kikubwa sana.
Leo hii TAKUKURU imegeuka mbwa koko licha ya kupewa meno ya kuwang’ata wala rushwa, taasisi hii nayo imekuwa miongoni mwa watuhumiwa wa kupokea rushwa.
Rushwa wanayoipata au uoga walionao dhidi ya Papa na Nyangumi vinaiondolea hadhi taasisi hii inayotumia mamilioni ya fedha za walipa kodi kujiendesha.
Juzi nimesikia TAKUKURU imewatia mbaroni walimu wawili Faustin Robert na Josephat Mwasote wa Shule ya Sekondari ya Forest iliyopo mkoani Mbeya kwa tuhuma ya kudai na kupokea rushwa ya shilingi mia tano (500) kutoka kwa wanafunzi wao.
Kamanda wa TAKUKURU mkoani humo, Daniel Mtuka, alisema walimu hao wanatuhumiwa kwa kuunda mtandao au mradi wa kuvuna fedha kutoka kwa wanafunzi wanaofanya makosa.
Mwanafunzi anayefanya kosa hutakiwa kupewa adhabu ya viboko au nyingine yoyote lakini kama akitoa sh 500 adhabu husika humuepuka. ‘Kwenye udhia tumbukiza rupia’ ndivyo walivyofanya walimu.
Mwanafunzi asiyetoa kiasi hicho cha fedha hupewa adhabu kali zinazotolewa katika chumba maalumu walichokipachika jina la ‘Guantanamo.’
Guantanamo ni jela ya Marekani iliyopo nchini Cuba inayosifika kwa mateso makali kwa kila wafungwa au mahabusu waofikishwa hapo.
Binafsi nimesikitishwa na kitendo cha walimu wale, maana walichokuwa wakikifanya ni kinyume cha maadili ya taaluma yao, pia ni kosa la jinai.
Walimu wale wanajenga taifa a wala rushwa, mwanafunzi aliyelelewa katika maadili ya kutoa rushwa ili asamehewe au apate huduma fulani kamwe hataichukia rushwa. Huyu atakuwa mtoa na mpokea rushwa jasiri.
Pamoja na kulaani walichokifanya walimu hao bado nina shaka na uwezo wa TAKUKURU katika utendaji kazi, hawa ni wepesi zaidi kuwashughulikia wanyonge kuliko vigogo wanaoiba kwa kutumia kalamu.
TAKUKURU ilipoomba ipewe meno na baadaye ilipopewa nilitarajia ingewang’ata watoa na wapokea rushwa wote bila kujali wadhifa au uwezo wa kifedha wa mhusika.
Kwa bahati mbaya baadhi ya watendaji wa TAKUKURU wamekuwa sehemu ya kupokea au kulazimisha rushwa. Wameigeuza ofisi ya umma kuwa mradi binafsi.
Hawa wanafurahia zaidi wanaposikia tajiri au kigogo fulani kakumbwa na tuhumu za kutoa au kupokea rushwa, wakifika huko hudai wapewe chochote kwa lengo la kutolifikisha suala husika katika ngazi za kisheria.
Kilio cha TAKUKURU huko nyuma kilikuwa meno lakini baada ya kupewa hawaonekani kuyafanyia kazi hasa kwa matajiri, vigogo wa serikalini na taasisi za umma.
Najiuliza, yako wapi meno waliyopatiwa? Hivi waliotoa meno kwa TAKUKURU waliyachunguza meno yao kama ni mazima au yameoza?
Najua meno yaliyooza kamwe hayawezi kuwa na ufanisi unaotakiwa. Kama TAKUKURU walipewa meno ya aina hiyo kwanini viongozi wake waliyakubali ilhali wakijua hayataweza kuwasaidia?
Chombo hiki sasa kinataka kiwe na mahakama yake itakayoshughulikia masuala ya rushwa, hoja hii wanaishibisha kuwa mahakama za kawaida zimekuwa kikwazo kwao.
Wanadai zinachelewesha kesi, mimi sikubaliani na hoja ya TAKUKURU, hawa wakipewa mahakama yao watakuwa wala rushwa zaidi. Watawaonea, kuwakandamiza watu kama ilivyokuwa ikifanyika huko nyuma kwa polisi.
Polisi walikuwa wanakamata wahalifu, wanachunguza na wanaandaa mashitaka. Hapa watu walikuwa wakilia zaidi kwa kesi za kubambikiziwa lakini tangu Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka nchini (DPP), ikabidhiwe jukumu la kuandaa mashitaka angalau mambo yamebadilika.
Kwa hali tunayokwenda nayo sina shaka ipo siku TAKUKURU watapigwa mawe na wananchi kama wataendelea na utaratibu huu wa kuwakamata walimu wenye kuchukua sh 500 huku wakiwaacha mafisadi wanaokwapua rasilimali za taifa kwa kutumia kalamu zao.
Mikataba mbalimbali ihusuyo rasilimali za taifa imetawaliwa na rushwa, TAKUKURU wakipewa kazi ya kuichunguza hutoa majibu ya kutokuwapo na rushwa, hili si geni, si tumeliona katika Richmond.
Wananchi sasa wana mahakama zao, porojo za serikali pamoja na vyombo vyake zimewachosha. Wahalifu wakikamatwa mitaani wananchi wameamua kuwahukumu hata kama ni kinyume cha sheria.
Kwa hali inavyokwenda, kuna kila dalili wananchi wakaanza kuwahukumu wala rushwa bila ya kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria kama wawafanyavyo vibaka wanaokwapua simu.
Maeneo yaliyokubuhu kwa rushwa yanajulikana, huduma kwenye zahanati, hospitali na vituo vya afya hazitolewi bure kama inavyotakiwa, kuunganishiwa umeme inahitajika rushwa, kuajiriwa kunahitaji rushwa. TAKUKURU hawayaoni maeneo haya?
TAKUKURU ilikuwepo kwenye chaguzi za vyama vya siasa ambako rushwa zilikuwa nje nje lakini mwisho wa siku waliokamatwa ni ‘dagaa’, tena wachache. Papa na nyangumi wa kutoa rushwa waliendelea kuogelea kwenye bahari ya rushwa.
Wananchi wanashangazwa, inakuwaje TAKUKURU inashindwa kesi ilhali ilishiriki kikamilifu katika ‘mitego’ na hatimaye kuandaa vidhibiti alivyokamatwa navyo mhusika?
TAKUKURU wenyewe hawaonekani kusikitikia kushindwa kwenye kesi walizozichunguza, huu ni udhaifu na kama chombo hiki kikiendelea hivi ni afadhali kivunjwe kiundwe kingine kitakachowajibika ipasavyo. Kwangu chombo hiki hakina faida.
Share this article :
 
Support : Creating Website | SAMBA Template | HAKI LEO Template
Copyright © 2011. HAKI LEO - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by HAKI LEO Template
Imewezeshwa na Haki Leo Company