Polisi hawa wawe fundisho

gazeti la Habari Leo
JANA Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk Emmanuel Nchimbi, aliwasimamisha kazi maofisa Polisi watano na kumpa mwingine likizo ya mwaka mmoja, kwa tuhuma mbalimbali za kukiuka maadili na utaratibu wa Polisi.
Kati ya Polisi hao, aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Mbeya, Elias Mwita, aliyekuwa Msaidizi wake, Jacob Kiango na aliyekuwa Mkuu wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia Mkoa wa Mbeya, Charles Kinyongo walisimamishwa kazi kutokana na tuhuma moja.
Inadaiwa viongozi hao walikabidhiwa kidhibiti cha dawa za kulevya aina ya cocaine kilo 1.9, wakatakiwa kuipeleka Ofisi ya Mkemia Mkuu, badala yake, ‘wakachakachua’ na kupeleka chumvi na sukari.
Aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi mkoani Kagera, Peter Matagi naye amesimamishwa kazi na atafunguliwa mashitaka ya kijeshi, kutokana na kukabiliwa na tuhuma za kuwabambikiza kesi zisizo na dhamana wananchi 13 wa Kata ya Nyakasimbi, wilayani Karagwe katika Mkoa wa Kagera.
Wananchi hao inadaiwa walibambikizwa kesi ya ujambazi wa kutumia silaha, na walikaa mahabusu kwa muda wa miezi miwili, baadaye timu ya uchunguzi iliyoongozwa na Dk Nchimbi mwenyewe, ikabaini kuwa mashitaka waliyoshitakiwa, hayakuwa sahihi.
Pia, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi, aliyekuwa anasimamia ajira katika jeshi hilo nchini, Renatus Chalamila, amepewa likizo ya mwezi mmoja, kutokana na tuhuma za kutajwa mara nyingi kuhusika kuwatoza fedha vijana walioomba ajira Polisi ili awapatie kazi hiyo.
Tunaipongeza Serikali kwa ujumla na Dk Nchimbi binafsi kwa kuchukua uamuzi huo, ambao unalenga kuimarisha nidhamu ndani ya Polisi na kuimarisha haki na usawa kwa kila Mtanzania.
Tunaunga mkono hatua hiyo ya Dk Nchimbi, kwa kuwa ni muhimu katika kuiondoa Serikali kwa ujumla na Polisi kama taasisi, katika kizimba cha kulalamikiwa na wananchi kila siku, kwa ukiukwaji wa haki za wananchi na ukosefu wa maadili.
Hata hivyo, tunashauri moto huo ulioanzia Makao Makuu ya Polisi mkoani Dar es Salaam, ukaenda Mbeya na Kagera, uendelezwe katika mikoa mingine na hasa katika hili la kubambikizia kesi wananchi na kulazimishwa rushwa ili kupata ajira.
Hatusemi kwamba suala la dawa za kulevya halina uzito, hapana, tunaipongeza sana Serikali katika hilo kwa kuwa dawa hizi zinaharibu zaidi vijana, rika ambalo linategemewa leo kwa ajili ya ujenzi wa uchumi wetu.
Lakini, tunasisitiza mkazo zaidi pia uwekwe katika suala la kubambikizwa kesi na rushwa katika ajira, ambayo athari zake ni kwa wananchi wa kipato cha chini zaidi, na yamekuwa kama saratani isiyo na dawa, ambayo imekuwa ikichafua jina la Serikali.
Ni vigumu kusikia Mtanzania mwenye kipato kizuri amebambikiziwa kesi, au anatapatapa kutafuta ajira kwa kutoa hongo, kama ilivyo kwa Watanzania wenye kipato cha chini, ndio maana tunasisitiza ili kuimarisha imani ya wananchi kwa Serikali, masuala hayo yawekewe mkazo.
Tunashauri watuhumiwa hao, wachukuliwe hatua sahihi za kisheria na ziwekwe wazi, ili iwe fundisho kwa wote na tunatarajia pia wananchi na wanasiasa wataiunga mkono Serikali katika hili na kuipongeza, kwa kuwa ni hatua muhimu katika kuimarisha Polisi itakayozingatia haki na usawa kwa Watanzania.
Share this article :
 
Support : Creating Website | SAMBA Template | HAKI LEO Template
Copyright © 2011. HAKI LEO - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by HAKI LEO Template
Imewezeshwa na Haki Leo Company