Duru za kidiplomasia za Wamagharibi zimefichua kuwa, nchi hizo zinapanga mpango mpya wa kutekeleza operesheni za kijeshi nchini Libya. Kwa mujibu wa habari hiyo, baadhi ya nchi za Ulaya na Kiarabu ambazo zimekuwa na mkono katika machafuko nchini Libya, zinapanga njama mpya ya kuingilia kijeshi masuala ya ndani ya nchi hiyo ya kaskazini mwa Afrika, kwa kisingizio cha kupambana na makundi yenye kufurutu ada. Vyanzo vya habari vinaeleza kuwa, operesheni hiyo imepewa jina la ‘Maua ya Msimu wa Machipuo’ na kwamba zitafanyika kwa kisingizio cha kukabiliana na makundi yenye kufurutu ada ambayo hivi karibuni yameshadidisha vitendo vya utekaji nyara dhidi ya wanadiplomasia wa nchi tofauti nchini humo. Hata hivyo nchi zinazotazamiwa kushiriki katika operesheni hiyo, hazijatajwa, lakini imeelezwa kuwa, operesheni hiyo itafanyika katika maeneo makuu matatu ya Libya ambayo ni pamoja na magharibi, mashariki na katika bahari ya nchi hiyo. Aidha imeelezwa kuwa, katika operesheni hiyo, kutatumiwa ndege za kivita, mabomu ya kisasa na meli za kivita. Hiyo itakuwa operesheni ya pili kufanywa dhidi ya nchi hiyo, tangu kung’olewa madarakani utawala wa Kanali Muammar Gaddafi nchini Libya. Katika wiki za hivi karibuni Libya imekuwa ikishuhudia wimbi la mashambulizi dhidi ya wanadiplomasia wa balozi kadhaa mjini Tripoli.